-

-

-

-

-

Habari Mpya

Sunday, 3 August 2014

Sehemu ya tatu : Watanzania Madanguroni China, Munira alivyojikuta na ujauzito usiokuwa na baba



Wakati anasumbuka na masuala ya viza, alihisi kuwa na hali isiyokuwa ya kawaida, aliamua kununua kipimo cha ujauzito cha bei nafuu.

Kwa bahati mbaya aligundua kuwa alikuwa mjamzito ambao anahisi kuupata siku alipobakwa na Wanigeria wanne.

Munira anasema suala la yeye kushika ujauzito lilileta shida zaidi, kwani mwenyeji wake, Jacky alimweka kikao na kumsuta kwa hilo bila kujali kuwa alibakwa. Mmoja wa wanawake hao ambao walikuwa wakifahamika kama ‘Boss Lady’ alimshauri kuwa atamtafutia mwanaume ambaye atamsaidia kutafuta daktari ili watoe mimba hiyo.

Alipofika kwa daktari, alipewa vidonge tisa ambavyo alitakiwa kulipia Yuan za China 600 (zaidi ya Sh100,000). Hakuwa na fedha hivyo alitakiwa kuendelea kujiuza licha ya kuwa hakuwa amepona ili apate fedha hizo.

“Baada ya muda nilipata fedha hizo na nilipewa vidonge, ambavyo hata hivyo haviharibu mimba kwa wakati huohuo bali taratibu sana,” anasema Munira.

Muda wa kuishi Guangzhou ulikuwa umekwisha na Munira hakuwa amepata viza, ilimbidi aondoke. Lakini mwenyeji wake alimwambia ni lazima atafute fedha ya kulipia viza usiku uleule. Akimaanisha akajiuze usiku huo na kupata fedha kwa ajili hiyo.

Munira alilazimika kuingia mitaani usiku ule kusaka wateja kwa ajili ya kupata fedha za kwenda kuchukua viza hiyo Macau, jimbo jingine maarufu nchini China.

Mwenyeji wake alimwambia wakati anaondoka asubuhi siku inayofuata, asiondoke bila kumuaga.

Aliporejea usiku wa manane alijiandaa kwa ajili ya safari ya asubuhi yake, licha ya kwamba hakuwa amepata fedha za kutosha.

Kulipopambazuka alikwenda kumuaga mwenyeji wake kama alivyoambiwa, lakini alishangazwa na kitendo cha mwenyeji huyo kumnyang’anya baadhi ya vitu kama nguo na viatu alivyomnunulia wakati alipofika nchini humo.

Wakati akiondoka alisindikizwa na Mtanzania, msamaria mwema, ambaye alimpa Dola 400 za Marekani kama akiba na nauli ya Yuan 50, hivyo kuongezea katika fedha alizokuwa amepata usiku ule.

Macau ni ‘Boda la JK’
Munira alichukua treni ya kuelekea Macau, mpakani lakini aliambiwa akiwa huko anatakiwa atoke kwa saa 12 kila baada ya miezi mitatu ili atakaporudi, aanze kuhesabiwa tena siku za kuishi.

Macau ni jimbo ambalo Watanzania wanapata msamaha wa kukaa kwa siku 90 bila viza, hivyo mara nyingi siku zinapokaribia kuisha, Watanzania katika jimbo hilo huondoka kwa saa 12, kisha kurejea kama wageni ambao huanza kuhesabiwa siku zao upya.

Kutokana na urahisi huo wa kimaisha, Macau umebatizwa jina na Watanzania ambao wanauita ‘Boda la Kikwete’, wakimaanisha kwamba maisha yao katika jimbo hilo ni kwa hisani ya makubaliano baina ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete na Serikali ya China.

Wakiwa Macau, Watanzania huenda kuchukua viza nchi jirani ya Malaysia, kinyume na hapo hubaki Macau, wakisubiri majaliwa ya kupata viza au kurudi nyumbani.

“Nilipofika Macau nilipata shida, Wachina hawajui Kiingereza, nazunguka na begi langu, kumbuka bado sijapona baada ya kufanyiwa ule unyama,” anasema.

Anasema alifanikiwa kuvuka mpaka wa Macau kutoka Guangzhou, ingawa alipata shida kupita katika viunzi vya uhamiaji kutokana na sheria za China.

Akiwa hoi kwa kuchoka, alikutana na raia wa Somalia ambaye alimsaidia kujaza fomu, lakini hata hivyo hakuweza kumsubiri, hivyo Munira alibaki peke yake.

“Nilipofika katika kiunzi cha mwisho cha uhamiaji, nilihojiwa sana, maofisa uhamiaji walidai kuwa sura yangu ya sasa haifanani na iliyopo kwenye hati ya kusafiria, hivyo wakawa na wasiwasi na mimi,” anasema.

Munira anasema maofisa hao walimuuliza maswali mengi kama namba ya pasipoti, umri, majina matatu, mambo ambayo aliyajibu kwa ufasaha, lakini bado hawakuridhika na wakampeleka kwenye chumba maalumu cha polisi kwa mahojiano.

Huko, walimwambia afumue nywele alizokuwa amesukia na kumhoji kwa zaidi ya saa moja kabla ya kumruhusu.

Anasema ni kweli sura yake halisi ilikuwa imebadilika baada ya kukonda sana, kutokana na mateso aliyokuwa anayapata.

“Mwisho wa siku waliniachia, nikachukue teksi, lakini ilinipoteza. Bahati nzuri mbele kabisa nikakutana na msichana raia wa Urusi, alichukua namba yangu na akanielekeza sehemu niliyotakiwa kwenda, huo ukawa mwanzo wa urafiki wetu,” anasema.

Mjini Macau
Anasema alipofika eneo aliloelekezwa, katika hoteli kubwa iitwayo St Marol, aliwakuta wasichana wengi zaidi ya 200 wa Kitanzania ambao viza zao zilikuwa zimeisha muda.

Walikuwa ni wengi na wote walikuwa wanajiuza.
“Mji huo ni kama Zanzibar hivi. Ni pazuri na ni mji wa gharama sana kila kitu ni gharama, hata hivyo wateja hawakuwa wengi kama Guangzhou,” anasema.

Katika hoteli hiyo ya St Marol, wasichana 15 hadi 20 katika eneo hilo, huchangia gharama za chumba.

Alishuhudia wasichana wadogo kuliko yeye, ambao walimlalamikia wakidai kuwa nao wanaishi maisha ya kujiuza ili wapate fedha kinachowakwamisha ni kukosa fedha za nauli ya kuwarudisha nchini.

Munira aliamua kuwasaidia, hivyo alishauriana na mmoja wao aitwaye Candy kwamba warekodi sauti kwenye simu wakieleza adha wanazopata, kisha wazitume Tanzania kupitia WhatsApp ili wapate msaada wa kurudi nyumbani.

Anasema ujumbe ule wa sauti ulisambaa karibu kwa Watanzania wote wanaoishi Macau, China, Guangzhou na Hong Kong na kwamba wezao wa Macau waligundua kwamba sauti hiyo ni ya mmoja wa wasichana wanaoishi kwenye hoteli hiyo ndipo walipoamua kwenda kuwasuta Munira na Candy chumbani kwako.

“Kundi la wasichana wa Kitanzania zaidi ya 100 walifika kwenye chumba chetu, wakaanza kutusuta kwa nini tuliamua kutuma ujumbe wa sauti kama ule.”

“Walitaka kunipiga wakidai kuwa nawaharibia maisha yao kwani wanapata pesa za kujenga nyumba na kununua magari kwa kazi hiyo,” anasema.

Anasema yeye na Candy walipoona hali imekuwa mbaya, waliamua kukimbia. Munira kwa hofu, alibahatika kubeba hati ya kusafiria, tiketi na kadi ya manjano, akiacha nguo na baadhi ya mali zake.

Hata hivyo, walipofika njiani, Candy alibadili uamuzi na kuamua kurudi hotelini.

“Nilimshukuru Mungu kwa kunipa akili ya kuchukua vitu vitatu muhimu, nikampigia simu rafiki yangu Mrusi, ambaye alikuja kunisaidia na kunipeleka kuishi kwake.

….Itaendelea
  • Blogger Comments
  • Facebook Comments

0 comments:

Post a Comment

Item Reviewed: Sehemu ya tatu : Watanzania Madanguroni China, Munira alivyojikuta na ujauzito usiokuwa na baba Description: Rating: 5 Reviewed By: Unknown
Scroll to Top